Monday, December 17, 2012
Vatican yataka utafiti wa viinitete vya binadamu upigwe marufuku (2) "Ni kashfa dhidi ya thamani ya mtu" Califonia yakiuka sera ya Bush, yahalalisha utafiti huo Na Cosmas J. Pahalah
Alisema kuwa Vatican inaunga mkono ule utafiti juu ya seli shina zenye asili isiyo yakibayolojia kwa kuwa njia hii kama ilivyoonyeshwa na mafunzo ya kisayansi ya hivi karibuni, “hii ni njia nzuri, inayotia matumaini na njia ya kimaadili ya kupata misuli ya kupandikiza pamoja na matibabu ya kiseli ambayo inaweza kuwafidia wanadamu.
Kama Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili alivyosema, “katika tukio lolote, njia za kisayansi zinazoshindwa kuheshimu thamani ya binadamu na tunu ya mtu-nafsi lazima ziepukwe daima.
Ninafikiria hasa juu ya majaribio ya utafiti wa viinitete vya binadamu kwa lengo la kupata viungo vya kupandikiza: utaalamu huu kadiri unavyohusisha kuchezea na kuharibu viinitete vya binadamu, hauwezi kukubalika kimaadili, hata pale lengo lake linapokuwa jema katika lenyewe.”
Aidha Baba Mtakatifu anaendelea kusema,”Sayansi yenyewe inaonyesha kuwa zipo njia nyingine za utabibu ambazo zinaweza kufikia malengo husika bila kuhusisha viinitete, lakini kwa kutumia seli shina kutoka kwa watu wazima.
Huu ndio mwelekeo ambao utafiti unapaswa kufuata iwapo unataka kuheshimu thamani ya kila mtu, hata yule ambaye bado yupo katika hatua ya kiinitete.”
Askofu Mkuu Martino aliendelea kusema kuwa uunganishaji wa viinitete kwa ajili ya utafiti wa kibayolojia na kitabibu au kuzalisha seli shina vyote huchangia mashambulizi dhidi ya thamani na ukamilifu wa mwanadamu.
Alisema kuwa kustawisha kiinitete cha binadamu wakati mipango ya kukiangamiza inafanyika, kungeanzisha uharibifu wa makusudi wa uhai wa binadamu anayetarajiwa kwa kisingizio cha “uzuri” usiojulikana wa utabibu tarajiwa au ugunduzi wa kisayansi.
Aidha alisema kuwa jambo hili linachukiza watu wengi hata wale wanaopigia debe maendeleo ya kisayansi na utabibu.
Alisema uunganishaji wa viinitete huzalisha uhai mpya wa binadamu usioelekezwa kwenye ustawi wa baadaye wa mtu bali kwa utumiwaji na uharibifu, ni mchakato ambao hauwezi kuhalalishwa kwa sababu kwamba unaweza kusaidia wanadamu.
Pia Mhashamu Martino alisisitiza kuwa uunganishaji wa viinitete hukiuka vipengele muhimu vya haki za binadamu.
Alisema “tangu mwaka 1988, migawanyiko miwili ya ulimwengu imekua zaidi: wa kwanza ni umaskini na unyanyasaji wa kijamii, na mwingine unahusu watoto wasio zaliwa bado ambao wamefanywa kuwa vyombo vya majaribio ya kisayansi na kiteknolojia.”
Aliongeza “hapa kuna hatari ya kuwa na aina mpya ya ubaguzi, kwa kuendeleza mbinu hizi ambazo zinaweza kupelekea uumbaji wa watu wa kiwango cha nusu mtu, ambao kimsingi hulengwa kutumiwa na watu wengine.”
Alisisitiza kuwa “hili lingekuwa muundo mpya na wa kutisha wa utumwa. Kwa masikitiko, kishawishi cha kukiuka maadili bado kipo, hasa pale maslahi ya kibiashara yanakapojiingiza. Serikali na jumuiya ya kisayansi ni lazima iwe macho katika eneo hili.”
Wakati hayo yakiendelea, katika hatua ambayo inapingana na sera ya utawala wa Rais George W. Bush, jimbo la California nchini Marekani limeridhia sheria mpya inayolenga kufungua milango kwa watafiti wa seli shina za binadamu.
Gavana Gray Davis, alitia saini sheria hiyo kuruhusu utafiti wa namna hiyo kufanyika, utafiti ambao umekuwa ukipingwa vikali na makundi pinzani dhidi ya utoaji mimba pamoja na Kanisa Katoliki kwa sababu utafiti huo unahusisha matumizi ya mimba changa pamoja na viinitete.
Suala hilo lilitawala vyombo vya habari zaidi ya mwaka mmoja uliopita pale Rais Bush alipokataa kutoa fedha za walipa kodi kugharimia utafiti wa seli shina za viinitete vya binadamu.
Hata hivyo, waungaji mkono wa sheria hiyo ya California wanasema kuwa hatua hiyo itavuta wanasayansi ambao siku fulani wanaweza kufanikiwa kutibu magonjwa sugu kwa njia ya utafiti huo.
Waungaji mkono wa sheria hiyo ni pamoja na Christopher Reeve, ambaye amekuwa mwanaharakati wa utafiti huo tangu alipopata ajali na kupooza kuanzia shingo kwenda chini.
Reeve anaamini kuwa utafiti huo unaweza kusaidia kutibu ugonjwa wa kupooza unaomsumbua.
“Tangu seli shina za binadamu zilipotenganishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1998, mdahala wa kisiasa umekuwa na athari kwa wanasayansi,” alisema Reeve na kuongeza “inaumiza kutafakari kwamba ni hatua gani ambazo zingekuwa tayari zimepigwa iwapo utafiti huo usingezuiwa.”
Seli hizo ambazo hupatikana katika viinitete vya binadamu, ‘umbilical cords’ na ‘placentas’, zinaweza kugawanyika na kuwa aina yoyote ya seli katika mwili.
Wapinzani wa utafiti huo wanadai kuwa utafiti huo ni sawa na uuaji kwa sababu unaanzia na kuharibu viinitete vya binadamu, ambavyo tayari huwa ni binadamu hai.
Akiwa ndani ya ndege yake, ‘Air Force One’, Rais Bush akisafiri kwenda New Jersey pamoja na katibu wa habari wa Ikulu ya Marekani, Ari Fleischer ambaye mwanzoni alisema kuwa sheria ya California inatokana na haki ya jimbo hilo kuwa na sheria zake. Alisisitiza ‘Rais amesema kuwa kuna mamlaka ndani ya majimbo ya kutunga sheria zake,” alisema Fleisher.
Hata hivyo baadaye Fleisher alirekebisha maelezo yake na kusema “Rais anadhani kwamba sera zote za majimbo na za serikali ya shirikisho zinapaswa kukuza utamaduni unaoheshimu uhai, na kwamba anatofautiana na kile ambacho jimbo la California na gavana wake amefanya.”
Seneta wa jimbo hilo, Deborah Ortiz aliandika muswada unaoelezea kuwa California itaruhusu kwa uwazi kabisa utafiti wa seli shina za viinitete vya binadamu na kuruhusu uharibifu na utoaji wa viinitete hivyo.
Muswada huo unataka kliniki za urutubishaji kufanya hatua za urutubishaji wa invitro ili kuwataarifu wanawake kwamba wana uchaguzi wa kutoa viinitete vilivyoachwa bila kutumiwa katika utafiti.
Aidha muswada huo unamtaka mwanamke anayehusika na viinitete kukubali kuvitoa kwa maandishi na unapiga marufuku uuzwaji wake.
Ortiz na waungaji mkono wa mswada wake walisema kuwa utafiti huo ungeweza kusaidia katika upatikanaji wa tiba ya magonjwa sugu, kama vile ugonjwa wa ‘Parkinson’, ‘Alzheimer’ na maumivu katika uti wa mgongo.
Sheria hiyo itavuta watafiti “wazuri na mahiri” kwenda California na hivyo kukomesha uhamaji wa watafiti katika eneo hilo kwenda katika nchi ambazo jambo hilo linaruhusiwa, alisema profesa Larry Goldstein, wa Chuo Kikuu cha California, San Diego.
Naye mtafiti katika Chuo Kikuu cha California, Susanne Huttner, alisema kwamba kwa kuwa serikali ya shirikisho haitalipia utafiti huo, watafiti katika California itawabidi wawe macho ili kutenganisha utafiti huo na masomo mengine.
Naye Mwongoza filamu Jerry Zucker aliungana na Davis na Reeve katika kutangaza sheria hiyo mpya, akisema kuwa alijifunza juu ya utafiti wa seli shina baada ya kugundua kwamba binti yake mdogo alikuwa na ugonjwa wa kisukari.
“Baada ya kujua utaratibu kwa kina, tulianza kuuliza nini kingefanyika ili kutibu kisukari,” alisema na kuongeza “kila mtu alitwambia kwamba utafiti wa seli shina za viinitete ndiyo tumaini lake bora ili aweze kupona.”
Zucker alisema kuwa baada ya hayo mara moja aligundua kuwa “kikwazo kikubwa katika kutafuta tiba kwa binti yetu ni serikali yetu wenyewe.”
Baraza la Congress halijashughulikia muswada wa utafiti wa seli shina au muswada unaopiga marufuku utafiti huo na Ortiz alisema kwamba bado kulikuwa na swali juu ya iwapo sheria ya California ingefyonzwa na sheria za shirikisho.
Masuala yanayosubiri kushughulikiwa na Baraza la Congress ni pamoja na kuruhusu utafiti huo ama kuufanya kama kosa la jinai hivyo na kuwashitaki wale walioenda nchi za ng’ambo na kupata matibabu kutokana na utafiti wa seli shina.
Davis alisaini muswada mwingine unaifanya kuwa ya kudumu ile marufuku iliyokuwa ya muda dhidi ya utafiti kwa makusudi ya kuzalisha watu, alisema msemaji wake Steve Maviglio. Marufuku hiyo ya muda ilitarajiwa kuisha mwishoni mwa mwaka huu.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment